Pages

  • Latest News

    Sunday, 23 November 2014

    Ni gharika kwa watu zaidi ya 50 sakata la Escrow

    Dar/Dodoma. Moto wa kashfa ya ufisadi katika akaunti ya Tegeta Escrow unaoendelea kuwaka bungeni, sasa unaonekana kugeuka gharika inayoweza kuwakumba vigogo wengi zaidi na kuiweka Serikali ya Rais Jakaya Kikwete katika hali ngumu.
    Kashfa hiyo ya uchotaji wa Sh306 bilioni za akaunti ya Escrow, inahofiwa kuwakumba vigogo zaidi ya 50 ndani ya Serikali wakiwamo mawaziri, makatibu wakuu, wabunge, majaji na wakuu wa taasisi za Serikali waliohusika.
    Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa kutokana na kuwapo kwa idadi kubwa ya mawaziri na watendaji wa Serikali na mahakama, inatishia anguko la Serikali.
    “Kuna waziri (anamtaja) ameniambia ameangalia ile orodha ya watu wanaodaiwa kuchukua fedha hizo ni zaidi ya 52. Hofu yangu hili jambo likiingia bungeni na kujadiliwa huenda likasababisha kuvunjwa kwa Baraza la Mawaziri kwa mara nyingine,” alisema mbunge mmoja kutoka Kanda ya Mashariki.




    Wabunge wajipanga
    Mbunge mwingine kutoka Zanzibar (CCM), alisema kuwa anasubiri kwa hamu kuchangia katika mjadala huo ili waondoke wale wote ambao wamekwapua fedha hizo.
    Juzi, Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliitisha kikao cha mawaziri ambacho kilihudhuriwa na baadhi ya mawaziri na walifikia uamuzi kuwa suala hilo litajadiliwa ndani ya chama kabla ya kuingia ndani ya Bunge.
    “Kinachosubiriwa ni ripoti ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) halafu tutakutana wabunge wa CCM kabla ya kwenda bungeni,” alisema mmoja wa wajumbe wa kikao hicho.
    Pamoja na hali hiyo, wabunge katika makundi makundi kwa wiki nzima wamesikika wakijadili jambo hilo huku wakilihusisha na mbio za urais mwakani.
    Mbunge mmoja (jina tunalo) alisema kuhusishwa kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika sakata hilo kunatokana na mtuhumiwa mmoja ambaye ni kiongozi katika Wizara ya Nishati na Madini, kuwa mmoja wa meneja wake wa kampeni.
    “Hakuna mahali ambapo Pinda ameguswa moja kwa moja katika ripoti ya CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali) wala Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa), bali wanasema ni kwa sababu ya kampeni za urais na mhusika mmoja katika sakata hilo anatajwa kuwa kama Pinda akipata urais, yeye ndiye  atakayekuwa Katibu Mkuu Kiongozi,” alisema mbunge huyo kutoka upinzani.
    Jana Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu akizungumza na gazeti hili, alisema sakata hilo linatakiwa liishe kwa kuwa linaumiza uchumi wa nchi kwa kuwa mtambo wa IPTL ni matatizo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Post a Comment

    Item Reviewed: Ni gharika kwa watu zaidi ya 50 sakata la Escrow Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top